May 16, 2011

usanii wa wasirikali

tulidhaani wasanii ni wale tu wanofanya sanaa. kumbe wanasiasa na washikaji ndo wamekuwa wasanii zaidi. kila siku wanabuni mbinu mpya za kuiba. wananchi waaliwa hata kile kidogo walicho nacho.

du!! tutakoma ubishi. kwa sababu kikwete na wakali wake wametuletea mpya zaidi na wanatukweta bila hata ya huruma. hala hala yasije tokea kama yaliyomkuta acheampong ghana. kwa vijana wetu wasiojua historia, nazungumzia baada ya watu wake kumtoa kwenye kiti kijeshi wakamtupia lawama zote yeye wakidai kuwa aliruhusu uozo usambae na kuota mizizi na kuacha rushwa na wizi wa kimasomaso kuwa kitu cha kawaida.

chonde ndugu zangu. . .

May 10, 2011

zamu yetu kula

wanasiasa wanapeana wenyewe kwa wenyewe. akiiba hapa anahamishiwa kuleee! kwingine ambako hajulikani ili akaibe tena na zaidi ya mara ya mwisho.

Jan 2, 2010

abdulmutallab

huyu abdulmutallab toka nigeria sijui mwendawazimu au nini? washenzi washenzi kama huyu ndiyo wanaofanya kusafiri kwa ndege kuwe kugumu. kwa sababu lazima tu wamarekani sasa wataongeza nuksi kwenye safari. ubaya wake ni kuwa watakaopata tabu zaidi si waarabu peke yao bali pia wanaigeria na hasa wenye majina ya kiarabu.

tatizo kubwa zaidi ni kwamba na siye wasafiri wengine wengine tusiokuwa wanaigeria, waarabu au waislamu na wala tusio na majina ya kiarabu tutaonewa bila sababu na hakuna mmoja wetu mwenye sauti ya kulalamika akasikilizwa. kwani ukisema fyoko basi na wewe utakiona kilichomtoa kanga manyoya. uwe umeonewa au la. juwa wazima hawa wamarekani wakidhani wanalinda maslahi yao hawamjali mtu yeyote yule asiyekuwa wao. hata ulie machozi ya damu.

haya basi tuone itakuwaje.

May 21, 2007

wanyang'anyi

inasemekana hivi sasa ardhi ni rasmali kubwa sana bongo. ukweli ni kwamba siku zote ardhi ni raslimali, isipokuwa sasa ni mara dufu ya wakati mwingine wowote ule. kwa hiyo wasirikali wamekuwa wanyang’anyi zaidi. kwa kawaida wanavamia mashamba ya wachovu na kudai kuwa wanaweka mapori. wenye pesa wakikodolea macho sehemu yako basi ishaondoka unapopatikana upenyo.

ni kumpa mjumbe wa nyumba kumi kiasi kadhaa au kumnywesha kangara, chibuku au bia mbili tatu atie dole gumba. ukishtuka unaambiwa kwamba sirikali imeigawa sehemu yako kwa sababu umeshindwa kuihudumia. na huna pa kwenda. kwani kila utakapokwenda ni mizunguko mizinguo tu ndiyo haiishi. pengine unayeongea naye ni shemeji yake huyo bosi aliyemuhonga mjumbe.

“njoo kesho, bosi hayupo. njoo kesho … njoo kesho.” utachoka mwenyewe. kufuatana na niliyosikia na kushuhudia, nchi ya kikwete na hawa wezi wezi wengine hivi sasa haina tofauti kubwa na za zamani. watu wasio na chao wanakwetwa sana. inasemakana mkwete ana sehemu kubwa sana tu kisarawe au sehemu fulani, ambayo aliipata kimizengwe.

swali, je, watu waliokuwa wakiishi pale wameishia wapi? na walipata fidia ya kutosha au kuridhisha, kufuatana na walichopoteza? au ndiyo walifanyiwa kiini macho tu? na kama sivyo walilalamika wapi? walisikilizwa?

ni kweli kuwa hali hii iko afrika nzima. kwa mafno msumbiji mawazir walikuwa akinunua mabsha makubwa na ardhi na kuiwekeza hadi hapo bei itakapopanda halafu wanauza kwa faida ya ajabu. lakini tunazungumzia rasmi bongo. nchi ambayo inajigamba kwa kuwa salama na isiyo na shida za ubaguzi na matatizo ya uhasama wa kidini. ukabila. na matatizo mengine kama hayo. lakini, je, nani anayezungumzia unyang’anyi huu wa ardhi za walala hoi? kama kweli maeneo fulani hivi sasa (kutokana na maendeleo, makuzi na matanuzi ya jiji) si maeneo ya mashamba tena, kwa nini sirikali isiwaambie watu wauze sehemu zinazowashinda kujenga? badala yake wananyang’anywa maeneo yao na sirikali, ambayo inayauza na kutia ndani pesa.

hii ni amri ya sirikali aua watu fulani tu wajanja wajanja waliopewa majukumu ya kuangalia mashamba na ugawaji/ uuzaji wa mashamba na viwanja? je, huu si wizi wa kimasomaso? na yote hii ni kutokana na unyonge wa wale wanaochaguliwa na kuporwa haki zao. wenye pesa sehemu zao haziguswi kamwe. sasa haki na usawa viko wapi?

navyoona mimi sirikali ingewaambia watu kuwa maeneo yao hivi siyo mashamba tena na ya kuwa wanatakiwa wejenge nyumba za kuishi, iwapo watashindwa basi sirikali itazigawa sehemu hizo ili ziuzwe kama viwanja. halafu itakata asilimia ndogo ili kujilipa fidia kwa huduma ya kugawa mashamba kitaalamu kuwa viwanja. wala siyo kuuza tu mashamba ya watu na kubaki na pesa. huu ni unyang’anyi, dhuluma na kuwanyima haki wenye mashamba. kitu ambacho kimekua cha kawaida sana sasa bongo.

mwalimu alishindwa na ujamaa wake. sababu kubwa ni kuwa watendaji wa kanuni zake walikuwa wakitenda kinyume au shingo upande. kwani walikuwa wakiona uhondo unawapita tu hivi hivi walipofananisha na wenzao wa kenya na nchi nyingine. matokeo yake ukabaji usiotumia silaha na unyonyaji, ambao wengi waliupenda tokea enzi, ndiyo ukapewa nafasi na sifa zote kwa madai kuwa ujamaa ulishindwa na kurudisha nchi nyuma (kama alivyoda njonjo).

kweli kuna majumba ya maghorofa marefu ya chuma na vioo na watu wengi wana tv (za hali duni), magari ya kupendeza na kuvutia (kupendeza hakumaanishi ubora). kwa wengine, wengi wasioelewa na wenye akili finyu, haya ni maendeleao. lakini maendeleo hasa ni watu na siyo vitu.

swali, ukabaji huu utakaposhindwa, au wananchi wakichoka kuonewa na kunyanyaswa, sulushisho litakuwa nini?

sidhani tena, na ni wazi, kama watu watataka kurudia ujamaa baada ya kuonja buyu la asali ya unyonyaji na ukandamizi wa wenzao wasio kitu. halahala walio lala wasiamke. vinginevyo, hatimaye, vumbi na manyoya yakishatulia, mwenye nguvu ndiyo atakayebaki kasimama.

walio baki alamsiki.

Apr 29, 2007

viongozi jina

juzi niliona picha ya watoto wa kibongo wakiwa darasani (http://harakati.blogspot.com/). jambo la kusikitisha ni kuwa, inavyosemekana, mbunge wa sehemu hiyo ni mmoja kati ya waliootesha mizizi bungeni na mtu mwenye nafasi serikalini. lakini hakuna chochote alichokifanya hadi sasa. watu wake, ambao ndiyo waliomchagua na kuendelea kumchagua, hawaelewi lolote (na kama wanaelewa basi wanaogopa kusema). na si huyu mbunge tu, inasemekana kuna wengine walio na nafasi serikalini na kwingineko wanaotokea sehemu hiyo.

kama kweli huyu mbunge angekuwa alitaka nafasi ili alete maendeleo kwa watu wake, nini alichofanya miaka yote hii ya ubunge wake? na hii ni sehemu moja tu. nina uhakika hali hii ipo nchi nzima. ila kwingine bado hakujafichuliwa. sasa kama hawa viongozi si viongozi jina, basi ni nani? kwani kwa jinsi inavyoonekana hakuna lolote wanalolifanya kwa niaba ya wachovu. ni wazi wako bungeni, na kwenye nafasi nyingine, kama wanowamba ngoma tu. wanavutia upande wao. kama hali hii iko nchi nzima - na hakuna dalili za kuonyesha kuwa kuna tofauti kubwa sehemu nyingine - basi wanyalukolo watakoma ubishi. nchi iko na itabaki kwenye matope. kama gari inayozungusha magurudumu tu. haiendi popote. mabosi hawashuki kusukuma hata siku moja (ati suti ichafuke?).

niwazi kuwa watu fulani wananufaika zaidi ya wengine kwa jinsi hali ilivyo. na inavyoendelea kubaki hivyo ndiyo wanavyozidi kuvimbiwa. wakati wachovu wanazidi kufa kwa njaa na maradhi. dhahiri viongozi hawa hawaoni aibu wala kujisikia vibaya kwa kuwakandamiza ndugu zao. hali hii itaendelea mpaka lini?

Jan 15, 2007

tumeingiliwa

hali halisi

kweli kila mtu ana haki na uhuru wa kuabudu dini yeyote au anavyotaka. lakini, hii ni kwa maneno tu. hali halisi si kweli kwamba kila mtu anafuata dini anayotaka au kuipenda. au kuwa na haki ya kutofuata kabisa dini yoyote ile kati ya hizi nyingi za kigeni na zilizopewa umashuhuri.

ukweli uliowazi ni kwamba kuna watu wamejipa uwezo wa kimungu mungu. wengi wanasiasa au washabiki tu wadini wanaofuata na kuipigia debe dini fulani. wanajifanya na kujiona kama vile yesu kristo au muhamad, watukuzwa wa dini ya kikristo na ya kiislamu. kwa kuwa dini ni imani basi anayemfuata yesu, kwa sababu zake binafsi, na amfuate. vivyo hivyo anayemfuata muhamad. badala yake utaona wakereketwa wako sehemu hawana kazi bali kutetana na kujifanya kana kwamba wao ni wateuliwa wa kutiisha watu sheria za kiislamu na kikristo. wengi wa watu hawa wanazijua hizi dini kijuu juu tu. lakini wamekuwa watakatifu kuliko hata huyo yesu na mtume wa waislamu. mwenye siasa kali anafuga ndevu kwa kudhani kuwa inawapa thawabu zaidi. hii yote ni uamuzi wao. kwa nini wawalazimishe wengine kufanya kama wao? tena kwa mijeledi.

swali. hivi hawa ndugu zetu wanoleta unoko kwenye ukristu na kujifanya wajuzi wa dini hii, wangapi kati yao wanaojua kuwa jina la yesu ni jina tu la kawaida (ambalo hutamkwa hee-sus) katika nchi zinazongumza lugha ya kispanish? na wangapi wanaojua kuwa katika enzi za utumwa, au tuseme wazungu kuleta utumwa afrika, moja ya meli mashuhuri sana katika biashara hii ilijulikana kwa jina la jesus christos - jina la yesu kilatini? kasome.

dini hizi zote ni za kigeni, kwa jinsi tuzijuavyo na zilivyoletwa afrika. (kuna wataalamu wa historia wanaodai kuwa dini zote hizi zina asili ya kiafrika). waafrika walikuwa na imani zao na taratibu za kutimiza na kufuata kanuni za imani hizo. kulikuwa na sehemu ya kufanyia sala, maombolezi au tambiko. iwe kusali chini ya mbuyu. mkuyu. mugumo. au kando ya mtoni. waislamu wana taratibu zao na wakristo nao. sasa inakuwaje za wengine (ambazo ni ngeni) zionekane bora zaidi, na kumlazimisha kila mtu kuzifuata hizo, na kuzitelekeza zao za kijadi? kwa misingi gani?

hawa wanaolazimisha watu kufuata uislamu kwa mijeledi, walipewa na nani uwezo huu? kweli allah anakubaliana na itikadi hizo? na mtu anayefuata dini kwa kuogopa mijeledi, je, huyu ana imani au anafuata mkumbo kwa kuogopa njukuti? yaani kuchapwa mikwaju na mtumwa aliyekula akashiba msikitini?

na hawa wanojifanya walokole, ili wawachune na kuwala walala hoi senti zao, je? wakati wanapata pesa za omba omba wanajidai kuhubiri na kuwapotosha wafuasi wao. ni lazima, ili wapewe chochote na wafadhili toka ulaya na marekani, waonyeshe kuwa kweli wanahubiri na kuwaingiza watu katika ufuasi wa yesu, hivyo ni muhimu sana kwao kuwarubuni watu ili wawaonyeshe mabosi wao kuwa kweli "tunafanya kazi mliyotupa."

hii haina tofauti na wanasiasa wanaoendeleza na kukuza kasumba ya omba omba toka ulaya. wakipata marupurupu asilimia 90% wanaiacha ulaya walikochimbia hazina zao za wizi na kuleta sehemu ndogo sana ya walichopewa na wafadhili. (uliishawahi kusikia wakati fulani bongo mrema alitangaza kuanzisha mfuko wa kupiga vita ujanja ujanja. alitoa dola na paundi elfu kadhaa, huku akijigamba kwamba ni pesa alizopewa kama rushwa na watu fulani wakati akiwa ulaya ili afungue akaunti pale. je, unajua ule mfuko uliishia wapi?)

katika filamu moja ya marehemu mzee usmane sembene (mungu na mizimu wamuweke pema) - iitwayo guelwaar, ambalo ni jina la mtu aliyekuwa mpigania haki za watu wake - guelwaar anasema, "sote tunajua kuwa ukiweka mikono mbele na kukunjua kidole kimoja kwenye ngumi, unaonyesha njia au kuelekeza. lakini ukiweka vidole vyote wazi, basi unaomba. na mtu aliyezoea kuomba na kupewa kila siku anajua maneno mawili tu, jaali jef - au "asante sana" kwa kiwolof cha sunugal.

ni wazi kuwa pazia tuliyowekewa usoni ni nzito kiasi kwamba si rahisi kuona janja ya wanaojifanya wadini na wanasiasa wa uongo na kweli. sababu kubwa ya kuwaingiza kwenye siasa na dini siyo kuleta mabadiliko, bali kutunisha vitambi na mifuko yao.

tufumbue macho waajameni. iwe dini iwe siasa. tunapozugwa tushituke. au tuwe macho zaidi ili tusizugwe kirahisirahisi. dini ni imani. fuata dini unayotaka. fuata chama unachotaka au muunge mkono mwanasiasa umpendae. ila usinilazimishe mimi. ntafanya na kufuata kile moyo wangu unachonituma, ili muradi sivunji sheria na raha yangu haimbugudhi mtu mwingine. vinginevyo niache kama nilivyo. kama nina dhambi au nimetenda visivyo, basi ni juu yangu na mungu wangu. we usijidai polisi na hakimu kwa niaba ya mungu.

ndumila kuwili

hawa watu wanojifanya watakatifu, au kupewa utakatifu na wapambe wao, au watu wengine wengine tu, pengine majumbani kwao ndiyo kuna uovu usiosemekana. je, nani atakaye wahukumu wao? mara ngapi tunasikia kuhusu shehe nanihii kamdunga selemani au kijana fulani mtiifu na mwenye imani na ari kubwa ya kutaka kujua mafunzo ya kitabu kitakatifu? au ya kuwa shehe nonihino kawaweka kinyumba watoto wa kiume au wakike, ati wanafunzi wake. na, je, vipi kuhusu padri, father stephen lugomba, au buruda stanslaus rogue? wakatoliki wanatakiwa wasioe, lakini yeye ana kina dada kadhaa (wapenzi wa biblia wanaoimba kwaya) wanaompa burudani baada ya sala ya jioni?

ndumila kuwili hawa atawahukumu nani? maalim vikapu kashawapa amri vijana wa mtaa waende kona ya mtachoka na ufukweni kuwachabanga magumi watu wa kijiwe kwa sababu wana pepa sayo. kwa nini kuvuta bangi ni kuvunja sheria lakini kunywa pombe si kuvunja sheria? wa kijiweni wanapigwa vita ati saa zote wanalikoleza badala ya kijiendeleza kimaisha - wakati hakuna kazi hata kwa waliosoma, kwa sababu ya undugunization. mbona shehe kurandaranda (na kanzu yake ambayo zamani ilikuwa nyeupe) haulizwi? muhishiwa shehe mlawiti, au padri japhet kambong'oza, kapewa na nani haki ya kuwahukumu wavuta bangi, wakati yeye mwenyewe anavunja sheria zaidi na mdhambi yake ni makubwa kuliko? na kila jumangapi lazima apate chupa kadhaa.

wao wenyewe wanakwenda kinyume cha vitabu vyao vitakatifu. kama si undumila kuwili basi ni nini? na vipi bado wana uwezo wa kuwahukumu wengine kwa makosa ambayo wao wenyewe ndiyo waovu zaidi. shehe na padiri walevi zaidi ya watu wanaowatuhumu kwa niaba ya dini zao. ukiangalia picha hii ina kasoro gani?

wapi kwenye vitabu hivi vitukufu inasema kuvuta bangi si halali? au kunywa pombe ni halali? (wala usifikirie vipi, mimi sinywi wala sivuti). na wapi inasema kasisi au shehe anaruhusiwa kukata kiu mara moja moja, kuwainamisha watoto wasiojua kitu na kuwatubisha kinamna? kama ni halali kwa nini wasifanye wazi watu waone kimasomaso?

tumeingiliwa na mdudu wa akili anayetufanya tuchukiane na kuuana bila sababu kutokana na dini za watu. kina mama wanalazimishwa kuvaa maguoguo, ati kwa sababu shehe nanihii karudi toka pakistani na wanawake wakipakistani, iran na yemeni wote wanavaa hijab au burka. kwa hiyo wanawake wakibongo wote lazima wavae kama kina mama wakiafganistani au uarabuni.

sidhani kama hata mmoja wa hawa ataenda peponi. si mwislamu si mkristo. ataenda kwa misingi gani? labda awe kafuata dini kwa misingi ya kujiokoa binafsi na wala siyo kwa ajili ya kuonekana kuwa ni mdini mkubwa kuliko wote. wema wake na msaada wake ni kwa sababu anawajibika kibinadamu na ana uwezo wala si kwa ajili ya kupata thawabu.

swali, shehe anayekwenda kuhiji kwa nauli aliyoipata kwa biashara ya magendo au kumzika kalimanzila hela zake za dagaa, au njia haramu anazozijua yeye (na kisheria), anapata thawabu?

kabla hujamtupia jiwe mtuhumiwa kwa uasherati, jiangalie kwa makini wewe mwenyewe. ni msafi na umetakata kiasi hicho? na unatupa jiwe kama nani? ungekuwa wewe ndiyo unayetuhumiwa ungesemaje?

umeshaona dhahabu zinazoipamba vatican? je kuna mgodi wa dhahabu pale? maswali ni mengi tu. jiulize mwenyewe kabla ya kujitia kimbelembele na kufuata mkumbo. wapo wanaofuata dini kwa sababu ya imani zao. lakini pia ni wazi watu wengi wanafuata dini siyo kwa sababu ya imani bali woga wa kwenda motoni (kama hizi dini zinavyofundisha -na ni dini hizi mbili tu zinazofundisha kuhusu peponi na motoni ) ndiyo unaowafanya watu waingie mkumbo wa dini hizi. na kwa wengi ni maslahi wanayoahidiwa na dini hizi na vyama vyao. na wengine wamo tu kwa sababu babu zao waliingia uislamu na uskristo. na wala siyo kwa sababu dini hizi zinampeleka mtu peponi. imani na jinsi mtu yeyote yule anavyoishi kwa mifano bora, wema na ukarimu ndiyo inampeleka mtu peponi. kama kuna peponi.

dini yangu. naamini mungu. au miungu. awe olodumare. buda. nzambe. nkulunkulu. nyame. shango. nguluvi. jah - rastafari. au nanabizhou. usinong'one wala kunizungumzia, ati mkafiri. afrika hakuna makafiri. makafiri wako kwenye akili za wanaotunga haya maneno tu. mimi ngangali. ungangali wangu unatokana na kulindwa na obatala. ogun. na mizimu yangu (iliyoko nyumba nitu na kwingineko)na kwa uwezo wa muumba. au waumba. kwa sababu naamini mungu. au miungu. wangu anajua na kuongea lugha nyingi. si kiarabu tu peke yake. au kirumi na kizungu kingine. lugha zote ni zake. au zao. vinginevyo sala zangu. mizimu yetu. zingejibiwa vipi? mungu (awe mmoja au wengi) ndiyo dini pekee nayoijua.

hizi nyingine biashara tu.

Dec 24, 2006

utu wa mtu

kila nikiangalia pande mbali mbali za afrika, na hasa mijini, naona ubinadamu unazidi kupungua tu. watu hawawajali wenzao kama ilivokuwa enzi zile. vijijini ndiyo unaweza kuona bado watu wanaonyesha utu. ingawa nako kuna matatizo yake - elimu ya giza au mambo ya mazingara, kwa mfano, yako mbele sana. nachokiona kwa wingi ni ule uzungu wa kusema, "everybody for themselves and god for us all - kila mtu ajue lake mungu ndiyo wetu sote." huu ni usemi unaotia nguvu utengano. kwa hakika ni usemi wa kikabaila. ukabaila hushamiri kwa wachache wenye nguvu kuwakandamiza wengi wasio na kitu pia kuwanyima nafasi ya kujitoa kwenye kibano.

wakati nchi za kiafrika zinazidi kuwa fukara, kwa kukamuliwa na wababe wa kimarekani na wazungu wengine, viongozi wa kiafrika (vikaragosi wao) wanatuna wakati wananchi wao wanazidi kukondeana kwa umaskini. wakati huo huo nchi hizi hizi, zijulikanazo kama maskini kupita zote duniani (wakati viongozi wao ni kati ya matajiri kupita wote duniani), zina machimbo ya almasi, dhahabu n.k. ambayo huwatajirisha mabwanyenye wa kiyahudi, kiarabu na wazungu pasipo mfano. isingekuwa watu kama kina mobutu na wengineo wenye akili za kushikiwa kama yeye, waafrika wangeumia lakini si kiasi hicho. na isitoshe siyo kuumizwa na ndugu zao. kwa bahati mbaya viongozi wengi wa kiafrika wanataka wawe kama mobutu.

kwa mfano kulikuwa na habari kuwa raisi wa zamani wa tanganyika alinunua ndege ya kujirusha mwenyewe pale anapojisikia. wakati huo huo hospitali za serikali hakuna dawa (hospitali za kibinafsi hata kwenye ndoto haziingiliki). sitoshangaa kusikia wabongo wamekopa msemo wa wamarekani: maskini hawaumwi wanakufa.

wengine wanajidai kuvutia utandawizi kwa kukaribisha wawekezaji. tushawashitukia, janja yao tumeiona tangu juzi. ndo maana ukisema sana wanakukata kilimi. kwa bahati mbaya wengi wetu bado mabozo, wananunuliwa kirahisi kwa tv kubwa na mikweche ya riko (reconditioned automobiles) toka uarabuni na nchi kupe nyingine.

hala hala kesho kuna moto wajameni.